Matokeo ya utafiti wa Twaweza kuhusu Uchaguzi Mkuu yamepingwa na wasomi, wanaharakati na wanasiasa, akiwamo mgombea urais wa Chadema na Ukawa, Edward Lowassa ambaye ameuponda na kueleza kuwa matokeo halisi yatapatikana Oktoba 25.

Utafiti huo unaonyesha kuwa kama kura zingepigwa kati ya Agosti na Septemba, mgombea wa CCM, Dk John Magufuli angeibuka na ushindi wa asilimia 65, wakati Lowassa angepata asilimia 25.
 

Lakini wadau  wanasema utafiti huo haujaakisi hali halisi inavyoonekana kwenye mikutano ya kampeni, ambayo inaonyesha wawili hao wanachuana vikali kutokana na kukusanya mashabiki wengi.
 

“Watanzania tusipumbazwe na tafiti ambazo hatujashiriki. Tushiriki kwa mafuriko Oktoba 25, majibu ya kweli tutayapata,” alisema Lowassa kwenye akaunti yake ya twitter.
 

Kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika Jimbo la Ndanda jana, ikiwa ni muda mfupi baada ya Twaweza kutangaza matokeo ya utafiti huo, Lowassa alisema anashangazwa kwa kuwa wananchi wanaomuunga mkono ni wengi.
 

“Kuna utafiti wa kura ya maoni umetolewa ukisema eti Magufuli amepata asilimia 65 na mimi 25. Nawashangaa kwa kuwa wanaoniunga mkono wako wengi,” alisema Lowassa na kuwaoji wananchi wangapi watampigia kura katika uwanja huo.
 

Huku wakishangilia wananchi hao walimjibu Lowassa “Tutakupigia” huku wakinyoosha mikono juu.
 

Baadaye Lowassa alisema: “Tutawajibu kwenye kura tarehe 25 na hamuwezi kukosea kwa kuwa mnaziona mvi hizi. Nangojea mafuriko ya kura kutoka kwenu.”
 

Lowassa alijiondoa CCM baada ya jina lake kuenguliwa na Kamati Kuu na kujiunga na Chadema Julai mwishoni. Chama hicho kilimpa fursa ya kugombea urais, akiungwa mkono na vyama vingine vya NLD, NCCR-Mageuzi na CUF vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
  
Maoni  ya  Wadau

Mbali na Lowassa kutokubaliana na matokeo ya utafiti huo, watu  mbalimbali pia wameupinga utafiti huo.
 

Mwenyekiti wa Kigoda cha Taaluma cha Mwalimu Nyerere, Profesa Penina Mlama amesema matokeo ya utafiti wa Twaweza hayalingani na hali halisi ya kisiasa inavyoendelea nchini.
 

“Kile kinachoonekana huko nje ni picha mbili tofauti,” alisema Profesa Mlama.
 

Amesema licha ya kwamba Twaweza wamefanya utafiti huo kwa kutumia vigezo vyao, matokeo yasingeonyesha tofauti kubwa kati ya wagombea hao.
 

Kauli hiyo iliungwa mkono na Profesa Kitila Mkumbo ambaye alisema: “Matokeo halisi tutapata baada ya wananchi kupiga kura Oktoba 25.”
 

Wakati wadau hao wakizungumzia tofauti ya uhalisia wa hali ilivyo na matokeo ya utafiti, mhadhari wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom), Paul Loisulie aliwataka wapinzani kutopuuzia maoni hayo ya wananchi, hasa kutoelewa nafasi ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
 

“Wanaweza wakapuuzia utafiti huo kwa kuwa unampa ushindi Dk Magufuli, lakini sio hili la Ukawa si chama cha siasa kilichosajiriwa kwa sababu itakapofika Oktoba 25 watu wanaweza kwenda kwenye karatasi ya kupigia kura kutafuta Ukawa,” alisema.
 

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Richard Mbunda alisema licha ya kukosa uhalisia kwa hali ya kisiasa iliyopo, matokeo hayo yanaweza kuwa changamoto kwa Ukawa, kujipanga upya na kuangalia mbinu za kuongeza ushawishi kwa siku zilizobakia.
 

Hata hivyo, Mbunda alisema matokeo hayo hayawezi kutabiri ushindi wa urais kati ya Dk Magufuli na Lowassa.
 

“Haileti mantiki kwa mashabiki wa Lowassa halafu utafiti uonyeshe amepata asilimia 25 ya kura. Ningependa ufanyike utafiti mwingine ili kuondoa maswali yaliyopo kwa sasa,” alisema.
 

Wakili wa kujitegemea na makamu mwenyekiti wa Chadema, Profesa Abdalah Safari alisema matokeo hayo ya Twaweza ni sehemu ya CCM kutapatapa na utafiti aliouita “feki na wa kutengeneza”.
 

Profesa Safari alisema haiingii akilini, muungano wa Ukawa na Lowassa ukatoa asilimia 25.
 

“Nusu ya vijana tumeshiriki kampeni za kuhakikisha wanajiandikisha kupiga kura na hata utafiti wetu unaonyesha CCM watashindwa. Kwa hivyo wanatafuta kurubuni taasisi ziwatengenezee uhalali wa kukubalika,” alisema Profesa Safari.
 

Maoni kama hayo yalitolewa na Profesa Gaudence Mpangalla kutoka Chuo Kikuu cha Ruaha ambaye alisema ni matokeo ya propaganda za CCM.
 

Alisema Lowassa akiwa CCM, matokeo ya utafiti wa taasisi hiyo yaliyonyesha alikuwa anaongoza kwa ushawishi katika nafasi ya urais.
 

“Nina shaka na hiyo methodolojia waliyoitumia kwa kweli,” alisema Profesa Mpangalla.
 

Dk James Jesse, mhadhiri wa UDSM, Kitivo cha Sheria pia alikuwa na shaka na utafiti huo.
 

“Matokeo haya yanaonesha walihoji watu fulani walioandaliwa na hawakuhoji watu mchanganyiko,” alisema.
 

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Teofilo Kisanji (Teku), Stephen Mwakajumulo alisema kama Twaweza iliweka vigezo sahihi vya utafiti, basi upo uwezekano wa majibu kuwa sahihi.
 

“Kumbuka mwaka 2005 ilifanya utafiti wa aina hiyo na kueleza kwamba mgombea wa CCM Rais Jakaya Kikwete angeshinda kwa asilimia 80 na matokeo yake yakawa kweli,’’ alisema na kuongeza mara nyingi utafiti unafanyika ili kutafuta mwelekeo wa ukweli kwa kutumia vigezo muhimu.
 

Wanasiasa

Mgombea ubunge wa Jimbo la Bumbuli (CCM), January Makamba alilalamika kuwa utafiti huo umewapunguzia asilimia za ushindi kwani wanaamini itakuwa zaidi ya asilimia 65.
 

“CCM haishangazwi na matokeo hayo kwa sababu, Magufuli amefika maeneo ya vijijini zaidi kuliko mgombea yeyote, ameeleza sera zinazoeleweka na ana sifa za uadilifu lakini wanaojadili mabadiliko hawaendani na historia yao, mwonekano wao ndiyo sababu wananchi wamekatishwa tamaa na hoja zao,” alisema ambaye wiki iliyopita alitangaza matokeo ya utafiti uliofanywa na taasisi ambayo hakuitaja unaoonyesha kuwa Magufuli anaongoza kwa asilimia 69.
 

“Mafuriko ya (mgombea wa NCCR-Mageuzi mwaka 1995) Agustine Mrema na (mgombea wa Chadema 2010) Dk Willibrod Slaa hayajawahi kutokea hadi sasa. Haya yanayojitokeza kwa Lowassa badala ya kuwasaidia yanawadhalilisha kwa kuwa mgombea wao hana uwezo hata wa kujieleza jukwaani kwa hivyo matokeo hayo yanaakisi ukweli wa hali halisi iliyopo...sasa wanaopinga na wao waje na utafiti wao tuone.”
 

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema kabla ya kuzungumzia utafiti huo wataujadili kwa kina kuangalia mazingira yaliyotumika kuufanya.
 

“Kwanza tuone ulivyofanyika ndiyo tutatolea ufafanuzi,” alisema.
 

Katibu Mkuu wa chama cha Sauti ya Wananchi (Sau), Ali Kaniki alisema matokeo hayo hayawezi kuaminika kwa asilimia kubwa.
 

“Kuna taasisi Uingereza walifanya utafiti kama huo na chama cha Labour Party kilioneokana kuongoza sana, lakini hadi matokeo yanatangazwa kilianguka vibaya,” alisema.
 

“Lakini inatakiwa kuheshimu utafiti huo na tusidanganyike na hoja za mafuriko. Wanaojitokeza kwenye mafuriko siyo wote wanaopiga kura.”
 

Hata hivyo, Katibu Mkuu wa Chama cha Kijamii (CCK), Renatus Muhabi alisema matokeo hayo ni chanzo cha kuashiria hatari ya machafuko, hivyo kusingekuwa na sababu ya kutoa utafiti huo kwa muda mfupi uliosalia.
 

“Ukiangalia ndani yake kuna propaganda za kisiasa zinazochezwa na CCM na inaweza kutuletea shida. Watu wako kwenye presha sana nadhani ingekuwa sahihi kusubiria uchaguzi ufanyike tu.”
 

Mwenyekiti wa UDP mkoani Dar es Salaam, Joachimu Mwakitinga alisema hakuna uhusiano wa hali halisi na matokeo ya asilimia 65 kwa Magufuli. Mwakitinga ambaye ni mjumbe wa Kamati ya Mamlaka na Taratibu za Uendeshaji Uchaguzi, alisema matokeo hayo ni uchochezi wa kampeni unaoweza kusababisha madhara makubwa kwenye Uchaguzi Mkuu.
 

Wanaharakati

Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu(LHRC), Dk.Hellen Kijo-Bisimba alisema sampuli iliyotumika kwa matokeo ya utafiti huo inaweza kuwa imeathiriwa na mazingira ya maeneo husika. “Wakati mwingine sampuli inaweza kudanganya na kuwa tofauti kabisa na uhalisia wa hali ilivyo na wakati mwingine kuelezea uhalisia wenyewe.”
 

Mkurugenzi wa Taasisi ya Sikika, Irinei Kiria alisema sampuli ya Watanzania 1,848 ni idadi ndogo na isiyoakisi Watanzania milioni 23 wanaotarajiwa kupiga kura mwaka huu.
 

“Lakini pia, wiki mbili tangu kufanyika uchaguzi huo ni muda unaoweza kubadili upepo mkubwa wa kisiasa kwa hivyo haiwezi kuwa matokeo halisi kwa hali ya sasa.”
 

Kiria alisema matokeo ya utafiti huo kwa Lowassa na Magufuli ni sawa na usiku na mchana kutokana hali halisi ya kisiasa ilivyobadilika katika uchaguzi wa mwaka huu.
 

Mratibu wa Mtandao wa Watetezi za Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), Onesmo Olengurumwa alisema matokeo na hali ya kisiasa nchini yanaonyesha tofauti kubwa.
 

Mwenyekiti wa mtandao wa mashirika yasiyo ya kiserikali mkoa wa Arusha (Angonet), Petro Ahham alisema utafiti ni mzuri, lakini pengo la ushindi wa CCM ni kubwa sana.
 

“Kwa hali ilivyo sasa huwezi kusema kuna mshindi wa asilimia 65, labda tuelezwe walioulizwa maswali ni waliojiandikisha tu sio hawa tunaowaona kwenye mikutano,” alisema.
 

Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Tumaini Dar es Salaam, Alline Ngirwa alisema utafiti huo umeonyesha ni maeneo gani hasa ambayo wananchi wanakerwa, kwa hivyo utawasaidia katika kipindi hiki wanapojiandaa kuamua.
 

“Wananchi wanakerwa na huduma za afya, ukosefu wa maji na elimu duni. Kwa hiyo matokeo ya utafiti huu yanatoa mwangaza kwa wapiga kura na wagombea juu ya vitu wanavyohitaji kwenye serikali ijayo,” alisema Ngirwa.
 

Mkurugenzi wa taasisi ya Compas Communication, Maria Salungi alisema utafiti huo si matokeo ya uchaguzi na kwamba katika kipindi kilichobaki kuelekea Uchaguzi Mkuu, yanaweza kubadilika.
 

“Haya sio matokeo ya uchaguzi ni maoni ambayo yanaweza kubadilika kulingana na wagombea watakavyoendelea kufahamika zaidi kwa wananchi, hivyo jamii isipokee kama ndio matokeo halisi,” alisema
 

Alisema katika utafiti huo, wengi waliohojiwa walitoa majibu kulingana na wagombea kufahamika zaidi, kutokana na majina yao kutajwa mara kwa mara ikiwemo kwenye vyombo vya habari na mabango.
 
Alishauri vyama vinavyounda Ukawa kuwaelimisha wananchi ambao wanaamini kwamba siku ya kupiga kura, watachagua Ukawa chama ambacho hakipo.

Chanzo:Mpekuzi